Skip to content Skip to sidebar Skip to footer

Sababu Kumi (10) Zinazopelekea Wakamilishaji Kushindwa-2

Habari muuzaji bora kabisa  kuwahi kutokea,

Eneo la kukamilisha mauzo ndiyo eneo ambalo watu wengi huwa wanaliogopa. Usiogope kumwambia mteja kinachofuata baada ya hapa ni wewe kulipia bidhaa au huduma unayotoa.
Na ndiyo eneo ambalo ukilifanyia kazi basi utaweza kuongeza mauzo kwenye biashara yako.

Hakuna pesa inayoingia kwenye biashara pasipo muuzaji kumtenganisha mteja na pesa zake.
Pale mteja anapokulipa ndiyo ushindi hayo mengine yote ni chenga.

Ushindi kamili kwenye mauzo, ni wewe muuzaji kupata fedha na mteja kupata bidhaa au huduma.

Hapa ni sababu tano ambazo mtu akiweza kuzivuka, ataweza kuwa na mafanikio makubwa kwenye ukamilishaji wa mauzo.

Soma hapa makala iliyopita kupata sababu nyingine tano; Sababu Kumi (10) Zinazopelekea Wakamilisha -1https://www.mauzo.tz/sababu-kumi-10-zinazopelekea-wakamilishaji-kushindwa-1/

6. Kuiga wengine.
Bindamu ni viumbe vya hisia, huwa tunapenda kufuata mkumbo kwa kuangalia wengine wanafanya nini.
Licha ya wewe kupata mafunzo, lakini kulingana na mazoea ya kijamii, bado unajilinganisha na wengine na kuona yale mazoea ambayo yanafanywa na wengi huenda ndiyo sahihi na kile unachoishi wewe siyo sahihi.

Changamoto kubwa ni  kwamba  watu  wengi  wanaotuzunguka hawana  malengo yoyote  makubwa,  hivyo  hawaweki  juhudi  kubwa.  Wakiona mtu anaweka  juhudi  kubwa wanamkatisha  tamaa. 
Kwa  kuzungukwa  na  watu wa aina  hiyo  na  kuwaiga,  huwezi  kukamilisha  mauzo makubwa.

Hatua ya kuchukua hapa;  Epuka  kutumia  muda  wako na  watu  ambao hawana  malengo makubwa.  Epuka kuchukua  ushauri wa watu  ambao hawana  mafanikio  na  wala  hawaelekei kwenye  mafanikio.  Simamia  ndoto  zako na  weka  juhudi  kubwa  bila kujali wengine  wanasemaje  au  kukuchukuliaje.

7. Kukosa mpango wa kifedha.

Watu wengi wanaishi lakini hawana mipango ya kifedha. Wengi wanasukumwa na hela ya kula, wanafanya kazi wakipata hela ya kula wanaridhika na kushindwa kuweka juhudi kubwa.

Watu ambao hawana  mpango wa kifedha  kwenye  maisha  yao,  huwa hawana msukumo mkubwa wa  kukamilisha  mauzo.  Chochote  wanachopata wanaridhika  nacho kwa  sababu  hakuna  kikubwa wanachotaka  kupata.

Hatua ya kuchukua hapa; kuwa na mipango mikubwa ya fedha ili uweze kufikia mafanikio makubwa na tumia mauzo Kama njia ya kukusukuma wewe kuuza zaidi na kupata mafanikio unayotaka.
Malengo madogo ya fedha yanakufanya uridhike mapema na kuwa mtu wa kawaida. Jitoe ili uuze zaidi na upate fedha zaidi.

8. Kuchukua malalamiko kama mapingamizi.

Siyo kila mteja malalamiko yake  ni mapingamizi. Mwingine anataka tu asikilizwe.
Wakati mwingine waache wateja wajielezee kwa njia ya kulalamika, wewe kaa kimya wasikilize huku ukiwaangalia machoni na baada ya hapo watajisikia vizuri baada ya kulalamika.

Wako wateja ambao desturi yao ni kulalamika, na hakuna kitu ambacho watu wanapenda kama ukiungana nao kwenye malalamiko yao wanayopitia.

Unapaswa  kuchukulia  kila  wanachosema wateja  kama  malalamiko tu, mpaka pale  utakapojiridhisha  kwamba  ni  mapingamizi  ya  kweli.

Na  kwa  malalamiko, usijisumbue  kuyajibu,  mteja  hataki  uyajibu,  anataka  tu  kuonyesha  maumivu yake.  Kwa  malalamiko ambayo wateja  wanayatoa,  wajibu  unawaelewa,  kisha endelea  na  mchakato  wa kukamilisha  mauzo. 

Hupaswi  kutumia  nguvu  na  muda mwingi  kwenye  kitu  kisichokuwa  na  nguvu  kwenye  mchakato mzima  wa mauzo.

9. Upungufu wa zana za kukamilisha.

Kama  huna  njia  na  zana  za  kutosha  kuweza  kukamilisha  mauzo, hutaweza kukamilisha  mauzo. Utafanya mauzo kuwa magumu kwako, lakini ukiwa na mbinu mbali mbali zitakusaidia kufanya mauzo kuwa rahisi kwako.

Unahitaji  kuwa na  silaha  nyingi  ili pale  mteja  anapoleta pingamizi  lolote  unakuwa na  njia  ya  kulikabili hilo pingamizi.

Kwa kuwa uko kwenye mafunzo ya mauzo, usiwe na wasiwasi kwa sababu utaendelea kujifunza mbinu hizo.

10. Kikwazo kisicho sahihi

Wauzaji  wengi  huwa wanaona  wateja  ni  kikwazo pale  wanaposhindwa kukamilisha  mauzo.  Lakini  hiyo  sahihi,  kikwazo  cha  mauzo kamwe  huwa siyo mteja,  bali muuzaji  mwenyewe. 

Hiyo  ina  maana  kwamba  kama  unashindwa kukamilisha  mauzo,  tatizo siyo wateja,  tatizo ni  wewe  muuzaji. 

Kubali hilo  haraka  na  jitafakari nini  unafanya  kukwamisha  ukamilishaji  wa mauzo.  Chukua  hatua kwa vikwazo unavyoweka  kwenye  ukamilishaji  wa mauzo ili  uweze  kukamilisha  mauzo makubwa zaidi.  Kwa  kukubali wewe  ndiye kikwazo  utaweza  kuona  maeneo  unayokwamisha  ukamilishaji  wa mauzo.

Kwa mfano, kama huzingatii mambo 16 ya kuzingatia wakati wa mazungumzo ya mauzo kama vile kusifia wateja, kutoa ushuhuda, kujali maslahi ya wateja wako lazima yatapelekea mauzo kuwa magumu kwako.
Pale unapokuwa unashindwa kukamilisha mauzo, jiweke kitimoto wewe mwenyewe, pitia yale mazungumzo yako na mteja na kisha utaona wapi unakosea.

Mwisho, umeshazijua sababu zinazopelekea watu kushindwa kukamilisha mauzo. Hivyo unapokutana nazo jua namna ya kukabiliana nazo ili uweze kukamilisha lengo lako kuu ambalo ni kuuza.

Kauli mbiu yetu; ABC: ALWAYS BE CLOSING-MARA ZOTE KUWA UNAKAMILISHA.

Mwl.Deogratius Kessy
Makamu Mkuu wa CHUO CHA MAUZO.
makamu@mauzo.tz

Leave a comment