Skip to content Skip to sidebar Skip to footer

Siri kuu ya mauzo inayoenda kukuletea wateja wengi zaidi wa uhakika

Ndugu yangu, Unakumbuka siku ulipopata changamoto, ukaenda Kwa rafiki yako kumwomba msaada? Mara baada ya kukusaidia kupata utatuzi wa changamoto yako ukifurahia sana. Kila mara unapomuona unajisikia vizuri, ikiwa akiomba kitu ni rahisi kumsaidia maana aliwahi kukusaidia.

Kumbe, msaada ni kitu kinachotolewa kwa mtu mwenye shida ili kuiondoa au kutimiza haja yake. Sisi binadamu huwa tunapenda kujenga urafiki na watu wanaoonekana kutusaidia, kuliko wasiokuwa na msaada kwetu. Hili wala halihitaji maombi wala mafuta ya upako ili kulielezea. Lipo wazi, tunaona katika maisha na utendaji wetu.

Upande wa mauzo sasa; Je, unaijua siri kuu ya mauzo? Watu wote unaowaona wamefanikiwa katika kuuza zaidi wanaijua siri hii na kuitumia. Ndiyo maana kila siku wanazidi kuuza zaidi na kukuza huduma zao. Leo nataka nikuibie siri hiyo. Je upo tayari? Usiwe na wasiwasi, nimeandika makala hii kwa ajili yako.

Siri kuu ya kufanikiwa katika mauzo ni “kujua kitu ambacho mwingine anakitaka sana, kisha msaidie kukipata kitu hicho”. Kwa lugha nyepesi mpe msaada. Hiyo sio tu siri ya mafanikio katika mauzo, bali ndiyo falsafa kuu ya mauzo, falsafa ambayo ukiishi kila siku kwenye mauzo yako, kamwe hutakosa wateja wa kuwauzia.

Utakuwa na mamia ya marafiki ya mteja wako, utapokea simu na oda nyingi maana watu wanapenda kwa karibu na watu wanaowasaidia mahitaji yao.

Wajibu wako muuzaji ni kujua kile ambacho watu wanapenda na kujali kwenye kile unachowataka wanunue, kisha waonyeshe jinsi ambavyo kununua kile unachouza kutawapa kile wanachotaka.

Hapa ndipo wauzaji bora wanapotofautiana na wauzaji wasio bora. Wauzaji bora wanakazana kujua kile ambacho mteja anakitaka sana, kisha kumwonyesha mteja jinsi ambavyo atakipata hicho kupitia bidhaa au huduma wanayouza. Na kama wakigundua walichonacho hakiwezi kumsaidia mteja kwenye kile anachotaka sana, wanamweleza wazi. Hata kama kwa kufanya hivyo hawatamuuzia mteja, wanakuwa wamejijengea uaminifu mkubwa kwa wateja kitu ambacho kinawapa fursa nyingine nzuri zaidi.

Wauzaji wasio bora huwa wanakazana tu kuwataka wateja wanunue, bila hata kujua wateja wanataka nini zaidi. Wanatumia nguvu nyingi pamoja na mbinu za ulaghai ili tu wauze, kitu ambacho hakina matokeo mazuri, kwani hata wanapouza, wanakuwa wamewapoteza wateja wao.

Kuwapoteza wateja sio kitu tunachoshauri, maana tunataka ujenge nao ukaribu hawa wateja, uwe rafiki yao. Jua mahitaji yao, weka nguvu katika kuwahudumia zaidi. Wape huduma iliyo bora zaidi. Wahudumie zaidi ya matamanio au matarajio yao.

Kupitia kujua wanachotaka itakuwa rahisi kuweka nguvu maana utaweka nguvu palipo sahihi na wateja watafurahia. Maana wajibu wako mkuu ni kuwasaidia kuchukua hatua wakati wa uhudumiaji. Ukiwa unaowahudumia zaidi ya kawaida au matarajio yao, hutahitaji kutumia nguvu kubwa ya kujitangaza au kujielezea zaidi. Badala yake huduma yako ndiyo itajielezea kwa mtu mteja mwenyewe.

Mara zote, tengeza marafiki na sio wateja. Marafiki mara zote hununua kwa marafiki zao. Hiki ni kitu kingine unachopaswa kujua na kufanyia kazi. Wadhihirishie wateja wako kuwa upo kwa ajili yao na sio ajili yako binafsi. Hapo wataona upo kutatua matatizo yao na sio kuchukua pesa zao.

Je, katika huduma au biashara yako unatengeneza wateja au marafiki? Jifanyie tathmini, kisha chukua hatua.

Habari njema ni kuwa, kitabu Cha MAUZO NI HUDUMA kipo jikoni kinaandaliwa. Unafanya nini ili kuboresha na kuukuza urafiki huo kwa wateja wako? Vyote vipo ndani ya kitabu hicho. Endelea kutufuatilia hapa hapa ili uwe wa kwanza kupata kitabu hicho pindi kitakapokuwa tayari.

Imeandaliwa na Lackius Robert, Mjasiriamali, Mwandishi wa vitabu na Mkufunzi Msaidizi Chuo Cha Mauzo. Karibu tuwasiliane kupitia 0767702659 au mkufunzi@mauzo.tz ili uwe wa kwanza kupata makala na kitabu.

Hakika, mauzo ni huduma.
Karibu tujifunze na kuuza zaidi.

4 Comments

  • Charles
    Posted September 8, 2023 at 2:32 am

    Kwanza utahitaji kumsaidia mteja juu ya changamoto yake, maana mteja napokuja dukani ni sawa na mgonjwa ili umtibie anatakiwa umfanye akuamini na awe rafiki yako, mara nyingi unaweza kujikuta umemuuzia vitu nusu mteja na nusu akachukuwa sehemu ingine, kwa sababu hukuonyeaha kumjali juu ya kutatuwa changamoto yake bali ulijitazama wewe binafisi. Unapo mfanya mteja kuwa wakwanza kuliko pesa utajikuta anatowa na order kubwa kuliko ya mwanozni vinginevyo ukienda kinyume utamuuzia kimoja, hata kama kuna kitu anataka hauna muonyeshe kwa kumtafutia kwanza akipate ili shauku yake uikate na uweze kumfanya kuwa rafiki yako kila siku atakuwa mteja wako na atakuletea na wengine wateja.

    • Post Author
      Lackius Robert
      Posted September 15, 2023 at 1:55 am

      Sure, Upo sahihi Linda. Tuna kazi kubwa ya kuwa karibu nao ikiwemo kuwasaidia changamoto zao pamoja na kujali Maslahi Yao. Nimefurahi kukusikia, ubarikiwe sana. Karibu tujifunze zaidi

  • Dickson Donatus
    Posted September 8, 2023 at 4:50 pm

    Ahsante kaka kuna kitu nimejifunza hasa ktk kutafuta marafki ktt biashara ni swala la muhimu sanaaa, well done my brother

    • Post Author
      Lackius Robert
      Posted September 15, 2023 at 1:53 am

      Asante sana Kaka Dickson, Mungu akubariki sana. Karibu tujifunze zaidi.

Leave a comment